Morgan Tsvangirai analaumiwa na wengi kwa masiabu yanayomkumba
Minong'ono ilikithiri kwa miaka
mingi. Wengi wakasema sio mjanja . Anapenda kucheza Golf sana . Ndio ni
jasiri kwa uhakika , lakini mtu asiye na mikakati.
Huyu ndiye mwanasiasa aliyejaribu mara tatu kuwa rais wa Zimbabwe lakini hakuwahi kufua dafu hata siuku moja.
Morgan Tsvangirai, sasa anatupia
macho hali ya kusahaulika kisiasa kufuatia chama chake kushindwa vibaya
katika uchaguzi mkuu uliokamilika wiki jana, na kuna watu wengi wanahisi
kuwa alipaswa kushindwa.
Hata ikiwa madai anayoyatoa kuwa kura ziliibwa
na chama tawala ZANU-PF yatathibitishwa na majirani wa Zimbabwe wakitaka
uchaguzi kurejelewa, rais Robert Mugabe hajaona sababu kubwa ya kuhofia
upinzani mkubwa kwa utawala wake.
Sasa kwa nini Tsvangirai alaumiwe?
Wadadisi wanasema kosa kubwa ambalo yeye na
chama cha MDC walifanya, ni uamuzi wake wa kujiondoa kutoka
kinyang'anyiro cha mwaka 2008 kwa sababu ya ghasia zilizotokea baada ya
utata uliofuata uchaguzi huo na kujiunga na rais Mugabe katika serikali
ya Muungano.
Na kama wanavyosema , Tsvangirai alimuwezesha mpinzani wake kushikilia wadhifa wakati yeye mwenyewe hakuwa na ushawishi mkubwa.
Hatua ya Tsvangirai ilizua utata mkubwa na
kupingwa na washirika wake wa karibu wa MDC - ingawa kunao wanaosema
kuwa hatua yake ilikuwa sawa.
Wafuasi wa Mugabe wakisherehekea ushindi wake wiki jana
Zimbabwe ilikuwa katika hali ngumu - uchumi ulikuwa unaporomoka.
Kwa kujiunga na serikali ya Muungano, Tsvangirai alionekana kutojali maslahi ya wafuasi wake wakati yake akiyapa kipaombele.
Hata hivyo kosa kubwa ambalo Tsvangirai alifanya ni kutojitetea wakati akiwa katika serikali ya Muungano na Mugabe.
Uhusiano wa dhuluma
Katika siku ya kwanza ambapo makamanda wa jeshi
la Mugabe walipokataa kumpigia saluti kama waziri mkuu wa Zimbabwe,
Tsvangirai angeteta na kupinga hilo na kisha kuwaambia wanadiplomasia
waliokuja kwenye mkutano huo, walikuwa wanapoteza muda na kisha
kujiondoa kwenye mkataba wa kugawana mamlaka.
Lakini kwa kukosa kujiondoa, alimuonyesha Mugabe
kuwa angeendelea kuwa katika serikali ambayo haimpi heshima zake na
yeye ni mwanachama mwenye ushawishi mdogo katika serikali ya Muungano na
kuwa angestahimili dhuluma katika uhusiano wao ambao ulifika mwisho
wake wiki jana.
Bwana Tsvangirai badala yake aliendelea
kusisitiza umuhimu wa kupatanisha watu akiwa na matumaini kuwa Mugabe
angezingatia demokrasia.
Muungano tawala ulionekana kumdhulumu Tsvangirai lakini kwa nini hakujiondoa?
Lakini badala yake, Mugabe -alimzuia , akabadili
sheria akiendelea kushikilia mamlaka hadi alipoitisha uchaguzi mkuu kwa
maslahi yake mwenyewe .
Baadhi wanasema kuwa Tsvangirai angejiondoa
kwenye uchaguzi kabla ya uchaguzi kufanyika wakati ilipokuwa wazi kuwa
Mugabe hangetoa muda kwa wapiga kura kujiandaa kwa uchaguzi, mfano
kujisajili au hata kufichua daftari la wapiga kura ambalo wengi wanasema
lilikuwa na dosari nyingi.
Lakini badala yake Tsvangirai aliitikia wito wa Mugabe wa kufanyika uchaguzi ambao sasa anasema ulijaa makosa na wizi wa kura.
Je ilikuwa hatua nzuri au ilikuwa ishara ya kutojua au kujiamini kupita kiasi?
Wakati mmoja hilo swali litajibiwa na wakereketwa wa chama chake na mwishowe wapiga kura.